VICHWA VYA HABARI

Blogger Tips and TricksLatest Tips And TricksBlogger Tricks t>

Thursday, March 17, 2016

Naibu Waziri apiga marufuku eneo la Shule kutumika kibiashara


Naibu Waziri apiga marufuku eneo la Shule kutumika kibiashara
Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Selemani Jafo, ameuagiza uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, kufuta mawazo ya kubadilisha matumizi Shule ya Msingi Uhuru Wasichana kama eneo la kibiashara.
Aidha amemtaka Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Isaya Mngurumi, kutoa kipaumbele kwenye malipo ya fedha za likizo na kupandishwa daraja kwa walimu wa shule hiyo, kutokana na kufanya kazi kwenye mazingira magumu.
Pia amemuagiza Mkurugenzi wa Manispaa kuhakikisha kuwa Shule hiyo haikosi karatasi maalum za kuchapishia maandishi ya nukta nundu, kwa wanafunzi wasioona.
Naibu Waziri alitoa maagizo hayo Dar es Salaam, tarehe 17 februari 2016 wakati alipotembelea shule hiyo ili kufahamu changamoto mbalimbali zilizopo.
Alisema lazima maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, ya kutaka Shule ya Uhuru wasichana isibadirishwe na kutumika kwa matumizi ya kibiashara yatekelezwe.
Mheshimiwa Jafo aliitaka halmashauri hiyo kuboresha miundombinu ya shule ili iendelee kutoa elimu kwa watoto kwa sababu bado serikali inahitaji uwepo wa shule za kutosha.
“Kama bado mna mawazo ya kubadirisha matumizi ya shule ya Uhuru wasichana ni bora muyafute, nataka maagizo yaliyotolewa na Waziri Mkuu, yatekelezwe” alisisitiza.
Mheshimiwa Jafo ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kisarawe, alionyesha kusikitishwa na mazingira magumu wanayokabiliana nayo walimu wa shule ya Uhuru mchanganyiko, ambao wanafundisha wanafunzi wenye mahitaji maalum.
Kutokana na hali hiyo, Naibu Waziri alimuagiza Mkurugenzi na Ofisa Elimu wa halmashauri hiyo, kuongeza magodoro yanayotumiwa na wanafunzi hao kufanyia mazoezi.
Aliongeza kuwa, walimu wa shule hiyo wanapaswa kupewa kipaumbele kwenye malipo ya likizo pamoja na kupandishwa madaraja kutokana na kufanyakazi kwa moyo wa kujituma.
“Mkurugenzi sitaki kusikia malalamiko kuhusu kucheleweshwa malipo ya likizo au kupandishwa madaraja kwa walimu hawa.
“Wamekuwa wakifanya kazi kwenye mazingira magumu lakini kwa moyo wa kujitolea hivyo nataka wawe wanapewa kipaumbele zaidi kwenye maslahi yao” alisema.
Naibu Waziri alisema, serikali itatilia mkazo upatikanaji wa vifaa maalum vya kufundishia ili wanafunzi wenye mahitaji maalum waweze kusoma bila vikwazo vyovyote.
Aliwataka wazazi walio na watoto wenye ulemavu, kutowaficha majumbani bali wawapeleke shuleni kupata taaluma.
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Anna Mshana, alimpongeza Waziri Jafo kwa kufika kujionea changamoto zilizopo ili ziweze kufanyiwa kazi.
Alisema, wanafunzi wenye mahitaji maalum wanahitaji uwepo wa vifaa vya kutosha vya kujifunzia.
Shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1921, ina wanafunzi 64 wasioona, 22 viziwi pamoja na upofu, 79 wenye mtindio wa ubongo pamoja na wanafunzi watano wenye ulemavu wa ngozi. 

0 comments:

Post a Comment